Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan amefanya uteuzi kama ifuatavyo:…
Na. Theresia Mande – Singida
Imeelezwa kuwa Taifa la Tanzania kama ilivyo kwa Mataifa mengine linawategemea vijana katika maendeleo na hivyo ni wazi jitihada kubwa inahitajika katika kuwekeza kwa vijana hasa katika eneo la afya na elimu.
Hayo yamesemwa na mkuu wa wilaya ya Ikungi Thomas Apson akimwakilisha mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba ambaye alikuwa mgeni rasmi katika bonanza la uelimishaji Afya ya Uzazi kwa vijana kupitia michezo mkoa wa Singida.
Katika kilele cha bonanza hilo lililofanyika katika viwanja vya chuo cha uhasibu na shule ya msingi ukombozi vilivyopo mjini Singida Apson amesema kupitia bonanza hili litawezesha kuwa na vijana wenye nguvu ya kuwajibika katika maisha yao wenyewe, familia zao na Taifa kwa ujumla.
Awali afisa kutoka Wizara ya Afya Idara ya Afya ya uzazi mama, mtoto na vijana Jesca Masanja amesema Jumla ya vijana na watu wazima 1553 katika manispaa ya Singida wamepatiwa elimu ya afya ya uzazi na huduma mbalimbali ikiwemo huduma ya uchunguzi wa saratani ya mlango wa kizazi, chanjo ya uviko 19 na ushauri nasaha na upimaji wa virusi vya UKIMWI.
Nao vijana walioshiriki bonanza hilo la siku tano wamesema wamejifunza mambo mbalimbali yahusuyo afya ya uzazi na wamenufaika kwa kuimarisha afya zao kupitia michezo mbalimbali hivyo wanaishukuru wizara na wadau wengine waliofanikisha bonanza hilo.