skip to Main Content
Simu: +255 653 200 211 | Barua Pepe: info@buhafmradio.co.tz  

Na Mwandishi Wetu, Iringa

WAKALA wa Nishati Vijijini (REA) umesema utahakikisha unashirikiana na sekta binafsi katika kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora na nishati ya uhakika vijijini.

Mkurugenzi waTeknolojia za Nishati Jadidifu na Nishati Mbadala wa REA, Mhandisi Advera Mwijage alisema hayo baada ya kukagua maendeleo  ya mradi wa ujenzi wa umeme wa maji (kilovoti 2400) wa Idete wilayani Kilolo unaotekelezwa na Kampuni ya Lung’ali Natural Resources Co ltd.

Amesema REA mpaka sasa imeishatoa ruzuku ya shilingi bilioni 4 kwa mradi huo ulio chini ya Kanisa Katoliki mkoani Iringa ambazo zimetumika kwa utafiti wa mazingira, ujenzi wa bomba la maji na jengo lenye mtambo wa kuzalishia umeme (Power House).

Kutoka kushoto ni Mkurugenzi wa Teknolojia za Nishati Jadidifu na Nishati Mbadala kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Advera Mwijage, Mwenyekiti wa Kijiji cha Idete, Henry Lekuti na Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Lung’ali Natural Resources, Padre Luciano Mpoma wakijadili jambo wakati walipokuwa wakikagua maendeleo ya utekelezaji wa Mradi wa ujenzi wa umeme wa maji (kilovoti 2400) wa Idete wilayani Kilolo unaotekelezwa na Kampuni ya Lung’ali, Septemba 23, 2023. REA inafadhili Mradi huu ili kuwezesha kuongeza umeme katika gridi ya taifa.

Mhandisi Mwijage amebainisha kuwa REA ina wajibu wa kuwaunganisha wazalishaji wadogo na taasisi zinazotoa mikopo kwa riba nafuu ambapo Benki ya TIB imeikopesha kampuni hiyo ili ikamilishe mradi huo wa umeme kwa wakati na kuingiza kwenye gridi ya taifa.

“REA inafanya kazi na sekta binafsi katika kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora ya nishati vijijini na kuchangia katika
shughuli za uchumi zinazoongeza kipato kwa wananchi,” alisema Mhandisi Mwijage.

Aliongeza kuwa serikali peke yake haiwezi kufanya kila kitu hasa katika miradi ya maendeleo inayogusa wananchi na hivyo kutambua umuhimu wa ushiriki wa sekta binafsi.

Mkurugenzi wa Teknolojia za Nishati Jadidifu na Nishati Mbadala kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Advera Mwijage, akikagua maendeleo ya ujenzi wa Mradi wa ujenzi wa
umeme wa maji (kilovoti 2400) wa Idete wilayani Kilolo unaotekelezwa na Kampuni ya Lung’ali
Natural Resources Co Ltd, Septemba 23, 2023. Wakala wa Nishati Vijijini (REA) unafadhili Mradi huu ili kuwezesha kuongeza umeme katika gridi ya taifa.

Serikali imekuwa ikiipatia REA fedha  ili kuwawezesha kufadhili miradi ya wazalishaji wadogo binafsi wa umeme ili miradi hiyo ichangie katika kiasi cha umeme kinachozalishwa katika gridi ya taifa .

Mhandisi Mwijage  ameweka wazi umuhimu wa wazalishaji wadogo wa umeme, katika maendeleo ya wananchi, na kusema serikali itaendelea kushirikiana nao.

Akieleza zaidi, amesema kuwa miradi ya uzalishaji umeme wa maji inasaidia kupunguza uzalishaji wa hewa ya ukaa na inatunza mazingira hasa kwa kuwezesha kuachana na matumizi ya jenerata katika kuzalisha umeme.

“Miradi hii pia inaiongezea serikali kipato kwa kulipa kodi, kuzalisha ajira na kuwapa wananchi uhakika wa upatikanaji wa umeme  na hivyo kushiriki kikamilifu katika shughuli za  kujiongezea kipato,” alisema Mkurugenzi wa Nishati Mbadala na Teknolojia.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni inayozalisha umeme huo wa maji, Lung’ali Natural Resources, Padre Luciano Mpoma alisema wanatarajia kuanza uzalishaji wa umeme Januari mwakani na kwamba ujenzi unaendelea vizuri.

Taswira ya Mtandao wa Bomba la kusafirishia maji kupeleka kwenye Mtambo wa uzalishaji umeme katika eneo la Mradi wa kuzalisha umeme wa maji (kilovoti 2,400) Idete wilayani Kilolo, Mkoa wa Iringa, unaotekelezwa na Kampuni ya Lung’ali Natural Resources Co. Ltd. Wakala wa Nishati Vijijini (REA) unafadhili Mradi huu ili kuwezesha kuongeza umeme katika gridi ya taifa. Taswira hii ilichukuliwa Septemba 23, 2023 wakati wa ziara ya Mkurugenzi wa Teknolojia za Nishati Jadidifu na Nishati Mbadala kutoka REA, Mhandisi Advera Mwijage.

Mradi huo utakapokamilika amesema wananchi wa Idete na maeneo mengine watakuwa na umeme wa uhakika na hivyo kuweza kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na huduma za kijamii.

Naye Mwenyekiti wa Kata ya Kidete, Henry Kikoti  ameelezea shauku ya wananchi kutaka mradi huo ukamilike kwani utaenda kuwa suluhu kwa umeme wa uhakika kwani uliopo hautoshelezi mahitaji ya shughuli za kiuchumi hasa kutokana na maendeleo na uwekezaji wa wananchi katika nyanja mbalimbali za kiuchumi.

Back To Top
Buha FM · Buha FM Radio Sauti Ya Kigoma