skip to Main Content
Simu: +255 653 200 211 | Barua Pepe: info@buhafmradio.co.tz  

Na Immaculate Makilika –MAELEZO

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye amesema kuwa Sekta ya Posta ni huduma muhimu barani Afrika inayohitaji kuboreshwa zaidi ili iendeelee kutoa huduma kulingana na mazingira ya sasa.

Akizungumza leo jijini Arusha wakati akifungua Jukwaa la Wasimamizi na Watoa huduma wa Sekta ya Posta kutoka ndani na nje ya Bara la Afrika, Waziri Nape amesema kuwa wadau hao wamekutana nchini ili kujadiliana namna nzuri ya kuboresha sekta hiyo.

“Sekta ya Posta bado ni huduma muhimu katika utoaji wa huduma mbalimbali katika maisha yetu ya kila siku na mtakumbuka kuwa hii ni sekta kongwe hivyo wamekutana kujadiliana ili kuona namna ambavyo Wasimamizi na Watoa Huduma za Posta wanaweza kuendelea kuboresha huduma hizi za posta. Huu ni mwendelezo wa mikutano kadhaa na kesho hapa Arusha kutakuwa na kikao cha Mawaziri wanaosimamia Sekta ya Posta katika Bara la Afrika”. Amebainisha Waziri Nape.

Kwa upande wake, Posta Masta Mkuu wa Shirika la Posta Tanzania, Bw. Macrice Mbodo amesema mkutano huo ni fursa ya kubadilishana uzoefu pamoja na kujadiliana changamoto za pamoja zinazoikumba sekta hiyo na namna ambavyo wataweza kuzitatua kwa pamoja na kusaidia kukuza maendeleo ya nchi za Afrika.

“Kama Tanzania tumepiga hatua ambazo nchi jirani wanajifunza na tayari ziko nchi mfano Kenya na  Zimbabwe ambazo tayari nina mwaliko wa kwenda kwao baada ya uzinduzi wa jengo la Makao Makuu ya Umoja wa Posta wa Afrika hapa Arusha nitakutana nao kuwaeleza yale ambayo wanahitaji tuwasaidie”. Amesema Mbodo.

Back To Top
Buha FM · Buha FM Radio Sauti Ya Kigoma