skip to Main Content
Simu: +255 653 200 211 | Barua Pepe: info@buhafmradio.co.tz  

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Prof. Joyce Ndalichako amekipongeza kiwanda cha mbolea cha  ITRACOM Fertilizer Limited kwa kuzingatia sheria za kazi ikiwemo kuwapa mikataba wafanyakazi, Usalama na afya mahali pa kazi na kuwasilisha michango ya wafanyakazi kwenye mifuko ya Hifadhi ya Jamii kwa wakati.

Prof. Ndalichako ameyasema hayo Septemba 18, 2023 alipofanya ziara ya kutembelea  kiwanda hicho kilichopo jijini Dodoma kwa lengo la kukagua utekelezaji wa Sheria za kazi, ambapo amewataka wawekaji nchini kuiga mfano kwa ITRACOM.

Waziri Ndalichako amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuweka mazingira wezeshi ya  wawekezaji nchini , uwekezaji wa kiwanda hicho cha mbolea  umezalisha  ajira za awali 1,198 na kitakapokamilika ajira moja za  kwa moja 3500 zitazalishwa na ambazo sio za moja kwa moja zitazalishwa ajira 8000.

Mhe. Prof. Joyce Ndalichako akiangalia mbolea ambayo imefungashwa alipotembelea kiwanda  cha mbolea cha  ITRACOM Fertilizer Limited kilichopo Dodoma.

Naye, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mhe. Jabir Shekimweri ameahidi kuendelea kuimarisha mazingira wezeshi kwa wawekezaji ili uwekezaji wa kiwanda hicho uweze kukamilika kwa wakati  na kuwa na  tija kwa wananchi.

Mkurugenzi wa Uratibu wa Ndani wa Kiwanda hicho, Kimaramuziro Nkurikiye ameshukuru serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Samia kwa kuendelea kutoa ushirikiano kwenye ujenzi wa kiwanda hicho na kutatua changamoto zilizokuwa zinawakabili ikiwemo maji, Umeme, na Barabara.

Aidha, Katika ziara hiyo Waziri Ndalichako aliambatana na Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mhe. Jabir Shekimweri pamoja na viongozi na watendaji yake na Taasisi zilizochini ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Back To Top
Buha FM · Buha FM Radio Sauti Ya Kigoma