skip to Main Content
Simu: +255 653 200 211 | Barua Pepe: info@buhafmradio.co.tz  

Na Anita Balingilaki

Serikali kupitia Bodi ya Pamba nchini (TCB) imenunua  na kusambaza jumla ya ndege zisizokuwa na rubani 20 kwa ajili ya kunyunyizia dawa za kuua wadudu  kwa wakulima wenye mashamba makubwa.

Hayo yamesemwa  hivi karibuni na Mhandisi Kisinza Ndimu kutoka Bodi ya Pamba  wakati wa uzinduzi wa zoezi la unyunyiziaji wa dawa kwa kutumia ndege hizo ambao umefanyika kata ya Budalabujiga wilayani Itilima mkoani hapa na zina uwezo wa hekari 15 hadi 20 kwa saa.

Ndege hizo zimesambazwa kwenye baadhi ya  wilaya  zinazolima zao la pamba nchini lengo likiwa kuwawezesha wakulima kukabiliana na changamoto ya wadudu waharibifu wa zao hilo.

Kati ya ndege hizo, saba zimepelekwa mkoani Simiyu kwa ajili ya kunyunyizia mashamba makubwa ya pamba ambapo mkulima atanyunyiziwa shamba lake pasipo  gharama yoyote.

Mhandisi Ndimu amesema wamefanya majaribio katika wilaya ya Itilima kwa kutumia ndege hizo ambazo zitatumika kupulizia mashamba makubwa ya Pamba.

” Bodi ya pamba tumekuwa tukitoa pembejeo kwa wakulima, mbegu, viuatilifu pamoja ni pampu za kupulizia ambazo hubebwa mgongoni kwa hali ilivyo wakulima wengi wana mashamba makubwa, tumeona ili kurahisisha kazi tuwaletee ndege zisizo na rubani (drone)” amesema Mhandisi Ndimu.

Wataalam wa teknolojia za Kilimo wakiiandaa ndege kwa ajili ya umwangiliaji wa viwatilifu huku wakulima wakishuhudia teknlojia hiyo itakayosaidia kukabiliana na wadudu waharibifu katika zao la pamba nchini

Aidha amesema mashine hizo zitasaidia wakulima wa pamba kutumia muda mchache wakati wa kupulizia,huku akiongeza kuwa  pampu za kawaida mkulima alikuwa anatumia muda mwingi kupulizia na kuchoka hasa akiwa na shamba kubwa.

Mkaguzi wa Pamba wilaya ya Itilima Said Itaso amesema awali walikuwa wanakutana na changamoto ya upuliziaji kwa wakulima wakubwa wa pamba ambao walikuwa wanahitaji teknolojia ili kurahisisha zoezi la upuliziaji wa mashamba yao.

Itaso amesema changamoto kubwa aliyokuwa akikutana nayo  kwa wakulima hususan  wenye mashamba makubwa kuanzia ekari 10 hadi  50 wengi walitumia siku nyingi kukamilisha kisha zoezi hilo huku akiongeza kuwa ujio wa mashine hizo imekuja kwa muda mwafaka.

Nao baadhi ya wakulima kutoka Budalabujiga  wakaipongeza serikali huku wakisema kuwa ujio wa ndege hizo utawawezesha kuongeza tija kwenye uzalishaji wa pamba hatua itakayowaongezea kipato cha familia zao.

Mkoa wa Simiyu ni miongoni mwa mikoa inayolima pamba kwa wingi huku ikitajwa kuzalisha nusu ya pamba yote nchini.

Back To Top
Buha FM · Buha FM Radio Sauti Ya Kigoma