skip to Main Content
Simu: +255 653 200 211 | Barua Pepe: info@buhafmradio.co.tz  

Na. Mwandishi wetu

Imeelezwa kuwa, Tanzania imepunguza maambukizi ya UKIMWI kwa asilimia themanini na nane (88%) kutokana na vifo vitokanavyo na UKIMWI kupungua kwa  asilimia hamsini   (50%) kutoka vifo 64,000 mwaka 2010 hadi 32,000 mwaka 2020.

Hayo yamelezwa jana jioni Jijini Dodoma wakati wa mawasilisho yaliyohusu tathmini ya hali ya UKIMWI nchini katika semina ya kamati ya kudumu ya Bunge ya Afya na masuala ya UKIMWI kuhusu majukumu ya Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania.

Akiongea wakati wa wasilisho hilo Mkurugenzi wa Ufatiliaji na Tathmini TACAIDS Dkt. Jerome Kamwela, alisema tafiti  zinaonesha kuwa, Maambukizi mapya ya VVU kwa watu wazima miaka 15 na zaidi yameshuka kutoka 110,000 mwaka 2010 hadi 68,000 mwaka 2020 na Maambukizi mapya kutoka kwa Mama kwenda kwa Mtoto (Mother to child transmission) yameshuka kutoka asilimia 18 mwaka 2010 hadi asilimia 7 mwaka 2020.

Baadhi ya wajumbe wa kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na masuala ya UKIMWI wakifuatilia uwasilishwaji wa mada kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDSDktLeonard Maboko wakati semina kuhusu masuala ya UKIMWI iliyofanyika Bungeni Dodoma

Sambamba na hali hiyo, Dkt. Jerome amesema kuwa Serikali inatakiwa kuongeza nguvu katika eneo la kuzuia maambukizi mapya ya VVU  hasa kwa Vijana kwani zaidi ya theluthi  moja ya maambukizi mapya hutokea kwa vijana wenye umri kati ya miaka 15-24, hususan vijana wa kike.

Aidha amesema Serikali itaendelea kuweka jitihada katika kuzuia maambukizi mapya ya VVU na kuimarisha huduma za upimaji na matumizi ya ARV kwa makundi maalum, kuimarisha huduma za kuzuia maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto ili kutokomeza kabisa maambukizi hayo, Kuhamasisha upimaji wa VVU, kuanza ARV na kufubaza VVU  hususan kwa wanaume, vijana na watoto.

Alifafanua kuwa jitihada hizo zitasaidia kukomesha vifo vitokanavyo na UKIMWI, kutokomeza ubaguzi na unyanyapaa kwa WAVIU katika jamii na kuongeza mikakati ya usambazaji wa condom katika jamii.

Akichangia Mada hiyo mjumbe wa Kamati ya Kudumu Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI Mhe. Elibariki Kingu alishauri Serikali kupitia TACAIDS kuweka mfumo madhubuti, wa kuweza kuwafuatilia watumiaji wa dawa za kufubaza makali ya virusi vya UKIMWI kama zinavyofanya nchi nyingine za Afrika akiitolea mfano nchi ya Namibia ili kuweza kupata takwimu kirahisi na kuwasaidia watumiaji kuepukana na hali ya kupuuziaji matumzii ya dawa hizo.

Akiongezea kuhusu uimarishwaji wa mifumo ya TEHAMA katika uratibu wa Afua za UKIMWI nchini, Kaimu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile alisema ipo haja kuwekeza nguvu katika matumizi ya teknolojia kwa kuitumia mifumo ili kurahisisha ufuatiliaji wa matumizi ya dawa kwa WAVIU.

Kaimu Mwenyekiti ya kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na masuala ya UKIMWI Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile akieleza umuhimu wa teknolojia katika utekelezaji wa afya za masuala ya UKIMWI nchini, wakati wa semina ya kamati hiyo kuhusu majukumu ya TACAIDS.

“Tukitumia teknoloji na unique identification itasaidia kujua, maana kuna wakati wagonjwa huama kutoka sehemu moja kwenda nyingine au kuacha matumizi ya dawa za ARV, teknolojia itasaidia sana kujua na kufuatili maendeleo yao na kulisaidia taifa katika utekelezaji wa afua hizi za UKIMWI,”alisema Dkt. Faustine Ndugulile.

Awali akifungua semina hiyo kwa kamati ya kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI Mkurugenzi Mtendaji wa TACAIDS Dkt. Leonard Maboko alitoa historia fupi kuhusu chimbuko la ugonjwa wa UKIMWI na kusema uligundulika duniani mwaka 1981 mpaka kufika barani Afrika hatimaye Tanzania ambapo uliingia mnamo mwaka 1983 ambapo mgonjwa wa kwanza aligundulika kutoka mkoa wa Kagera hadi kufikia mwaka 1986 ulienea katika mikoa mingine nchini.

Dkt. Maboko aliongezea kuwa, Serikali imekuwa na mikakati madhubuti katika mapambano dhidi ya UKIMWI ambayo yameendelea kuzaa matunda na kuyafikia malengo yaliyokusudiwa.

Back To Top
Buha FM · Buha FM Radio Sauti Ya Kigoma