Asema hadi sasa imeshawekeza dola za Marekani bilioni 10 WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema hadi…
Na. Mwandishi wetu- Kigoma
Serikali ya Ubelgiji kupitia shirika la kuhudumia wakimbizi UNHCR imetoa kiasi cha Euro milioni nne sawa na takribani shilingi bilioni kumi za Tanzania kwa ajili ya kuwezesha utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimazingira katika eneo linalohifadhi wakimbizi mkoani Kigoma kupitia mpango wa pamoja wa umoja wa mataifa kwa ajili ya mkoa wa Kigoma.
Akitoa taarifa katika halfa ya uzinduzi wa mradi wa kuhifadhi mazingira dhidi ya mabadiliko ya tabia nchi uliofanyika mjini Kigoma, Balozi wa Ubelgiji nchini Tanzania Mh. Peter Huyghebaert amesema serikali ya Ubelgiji imetoa fedha hizo baada ya kuombwa na UNHCR Tanzania kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wa mkoa wa Kigoma waliopokea wakimbizi
Balozi Peter amesisitiza kuwa nchi ya Ubelgiji pamoja na nchi nyingine za umoja wa ulaya zinatambua wema unaofanywa na watanzania katika mkoa wa Kigoma kwa kupokea na kuwapa hifadhi wakimbizi kutoka nchi za Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na kwamba kutokana na ujio wa wakimbizi hao zipo athari mbalimbali hususani za kimazingira.
Amesisitiza kuwa, ufadhili uliotolewa utasaidia kukabiliana na athari za kimazingira ikiwemo uoteshaji na upandaji miti, uanzishwaji wa miradi ya nishati mbadala ili kupunguza matumiti ya miti kwa ajili ya nishati ya kupikia kwa wenyeji pamoja na wakimbizi wenyewe katika kambi za Nduta na Nyarugusu
Kwa upande wake Mwakilishi wa UNHCR nchini Tanzania Bi. Mahoua Parums pamoja na kushukuru ushirikiano mzuri uliopo baina ya serikali mkoani Kigoma, amesisitiza kuwa mradi huo wa kukabiliana na changamoto za kimazingira katika maeneo yanayohifadhi wakimbizi ni mhimu sana kwa maslahi ya wenyeji na wageni.
Parums anasisitiza kuwa ili kutatua changamoto mbalimbali zinazotokana na kuhifadhi wakimbizi ni mhimu wadau mbalimbali waunganishe nguvu katika kuisaidia jamii ya watanzania mkoani humu kutatua changamoto za kiuchumi, kijamii na kimazingira ili kuwa na maisha bora na ujirani mwema baina yao na wakimbizi.
Inaelezwa kuwa kutegemea misitu kwa ajilii ya nishati miongoni mwa wenyeji na wakimbizi kunatajwa kuwa achanzo cha migogoro na hali ya sintofahamu miongoni mwa watanzania na wakimbizi jambo linalopelekea kuwepo kwa umhimu mkubwa wa kutafuta suuhisho la utegemezi wa kuni na badala yake miradi mipya ya nishaji jadidifu na nishati mbadala iwe chachu ya kupunguza athari za wakimbizi kwa mazingira na kujenga amahusiano mazuri baina yao na wenyeji.
Mkurugenzi wa wakimbizi nchini Tanzania Bw. Sudi Mwakibasi ammekiri kuwa kwa sasa hali si nzuri kutokana na kuwepo kwa ongezeko kubwa la wakimbizi ambao tegemeo kuu la nishati ya kupikia ni kuni zinazotokana na misitu na kwamba ufadhili unaotolewa na wadau utakuwa chachu ya kuimarisha mahusiano baina ya wakimbizi na wenyeji na hivyo kupunguza migogoro.
Akishukuru nchi za umoja wa Ulaya kwa misaada mbalimbali zinazotoa kwa mkoa wa Kigoma, mkuu wa mkoa huo Bw. Thobias Andengenye amekiri kuwa eneo hilo linahitaji jumuiya ya kimataifa katika kutekeleza mipango mbalimbali ya kuboresha Maisha ya wananchi na kupunguza athari zinazotokana na wakimbizi
Mabalozi wanne kutoka nchi za umoja wa ulaya zinazofadhili misaada kwa wakimbizi nchini Tanzania pamoja na Japan wakifuatana na maafisa wawakilishi wa mashirika ya umoja wa mataifa pamoja na ubalozi wa Marekani wapo mkoani Kigoma kwa ziara ya siku tatu kutembelea miradi ya maendeleo inayotekelezwa na umoja wa mataifa kwa hisani ya nchi hizo ambapo wamezindua rasmi mpango wa kunusuru mazingira na mabadiliko ya tabia nchi kwa kupanda miti.